Wednesday, June 05, 2013

Zifahamu sababu za ugumbwa kwa wanaume


Kwa ufupi
  • Taasisi ya Taifa ya Afya ya nchini Marekani (NIH) inaeleza kwamba sababu za jumla za ugumba ni umri na  asilimia nne ya wanaume wenye umri wa miaka 50  na kuendelea wanaweza kuwa na tatizo hilo wakati nusu ya wanaume wenye umri wa miaka 75 wanakumbwa na ugumba.

Ukosefu wa nguvu za kiume nchini twaweza kusema  ni janga. Hii ni kutokana na tafiti zilizowahi kufanywa na pia kuzagaa kwa vibao vya matangazo kuhusu dawa au tiba ya tatizo hilo.
Tatizo hili halipo kwa wazee kama ilivyodhaniwa zamani, bali hata kwa vijana, wake kwa waume wamekuwa wakiguswa na tatizo hilo.
Sababu nyingi zimewahi kuanishwa kuchochea ugumba kwa wanaume ikiwamo maradhi, kutazama luninga kwa muda mrefu na kutofanya mazoezi.
Hivi karibuni wataalamu katika Jarida la Jinsia na Tiba  la nchini Uingereza, lililochapishwa Januari lilieleza sababu kuu duniani zinazochochea ugumba kwa wanaume iwe wa muda mrefu au wa kudumu.
Taasisi ya Taifa ya Afya ya nchini Marekani (NIH) inaeleza kwamba sababu za jumla za ugumba ni umri na  asilimia nne ya wanaume wenye umri wa miaka 50  na kuendelea wanaweza kuwa na tatizo hilo wakati nusu ya wanaume wenye umri wa miaka 75 wanakumbwa na ugumba.
Daktari wa Upasuaji na Nguvu za Kiume katika Chuo Kikuu cha Tiba cha Maryland,  Dk Andrew Kramer anasema karibu nusu ya wanawake na wanaume wote duniani wanakosa nguvu za kiume aidha moja kwa moja au katika nyakati fulani za maisha yao.
Madereva
Dk Kava anasema wakati wa zama za chuma ilibainika kwamba wanaume wanaoendesha baiskeli kwa muda mrefu, waendesha farasi na madereva wa magari kwa muda mrefu wamo hatarini kukosa nguvu za kiume.
Jarida la tiba lilifanya utafiti na kubaini kuwa asilimia nne ya wanaume wanaoendesha baiskeli kwa saa tatu au zaidi kwa wiki wanapata matatizo ya nguvu za kiume.
Anasema unapokaa kwenye gari, farasi au baiskeli kwa muda mmrefu unaweka nguvu katika neva na mishipa midogo inayobeba damu kwenda katika uume.
Anafafanua kwamba uendeshaji wa vyombo hivyo kwa muda mrefu unaharibu mishipa midogo na damu haiendi inavyotakiwa katika uume.

Maradhi ya fizi
Pengine unaweza kujiuliza fizi na nguvu za kiume vina uhusiano gani? Wataalamu wa Afya wanasema, kuwa na matatizo sugu ya fizi au fizi zilizoathirika kunaweza kuongeza hatari ya mtu kukosa nguvu za kiume.
 Watafiti wanasema maradhi ya fizi ni dalili za afya dhaifu na inahusishwa na ongezeko la maradhi ya moyo na upungufu wa nguvu a kiume.
“Maradhi ya fizi yanaweza kusababisha matatizo katika kusukuma damu, hivyo matatizo hayo yakizidi, yanaweza kusababisha damu ishindwe kufika katika uume,” anasema Bruce Kava, Mwenyekiti wa Tiba ya Mfumo wa Mkojo katika Chuo Kikuu cha Tiba cha Miami Miller.
Kisukari ni sababu nyingine na Taasisi ya Taifa ya Afya ya nchini Marekani inasema wanaume wanaougua maradhi ya kisukari wana hatari mara tatu zaidi kukosa nguvu za kiume kuliko wanaume wasio na maradhi hayo.
Dk Kramer anasema  sukari isipodhibitiwa katika damu, inaharibu neva na misuli midogo inayodhibiti kusimama kwa uume. 
Pia asilimia 61 ya watu wenye msongo wa mawazo hawawezi kuwa na nguvu za kiume.
Taarifa kutoka Kliniki ya Cleveland inaeleza kwamba msongo wa mawazo unasababisha mambo makubwa zaidi katika mwili na unaweza kuathiri kwa kiasi kikubwa  nguvu za kiume.
Msongo wa mawazo unasababisha Kemikali za seli za ubongo zinazowasiliana katika kusisimua mtiririko wa damu hadi katika uume kushindwa kufanya kazi.
Pia Dk Malebo anasema wanaume hukosa nguvu za kiume kutokana na msongo wa mawazo  ambao unatokana na migogoro ya kifamilia, ufukara au imani za kishirikina.
Dk Kramer anasema dawa za saratani na zile za kuondoa vipara zinazotumiwa zaidi na wanaume zinaweza kusababisha madhara ya nguvu za kiume.
Mkuu wa Kitengo cha Utafiti wa Tiba Asilia katika taasisi ya utafiti wa tiba nchini (NIMR), Dk Hamis Malebo anasema  sababu kuu za ugumba kwa Tanzania ni mfumo wa maisha.
 Anafafanua kwamba aina za vyakula, mtindo wa maisha, msongo wa mawazo na utofauti katika vichocheo ni baadhi tu ya sababu za ukosefu wa nguvu za kiume.
“Baadhi ya vyakula vina kemikali ambazo zinapoingia katika mwili zinaharibu usukumwaji wa damu katika uume” anasema dk malebo ambaye aliwahi kufanya utafiti kuhusu ugumba.
Samaki na maziwa ni sababu
Kwa mfano, watu wengi hununua maziwa ya ng’ombe ambayo yamechomwa sindano siku mbili au moja nyuma bila wao kufahamu
“Au samaki wanaovuliwa kwa kemikali na mabomu ni sababu zinazochangia kwa kiasi kikubwa ukosefu wa nguvu za kiume,” anasema.
 Anasema kemikali hizo zinaathiri uzalishaji wa vichocheo na usukumwaji wa damu kutoka katika moyo hadi katika uume.
Anashauri  kuwa ili kuepukana na tatizo la nguvu za kiume  hasa kwa wale wenye msongo wa mawazo sulushisho ni kubadili mfumo wa maisha.
“Kuhusu mvurugiko wa homoni, udhibiti wa serikali unahitajika. Maziwa ya ng’ombe, yanayokamuliwa wakati ng’ombe amechomwa sindano pamoja kemikali za kuvulia samaki zidhibitiwe,” anasema.
Anasema uwiano mbovu wa vichocheo unaweza kutibika hospitali kwa dawa zinazorekebisha mfumo huo  na pia zipo dawa za asili.
Mmea wa Alikisusi (licorice) kwa kisayansi Glycyrrhiza Giabra una uwezo wa kutengeneza uwiano wa vichocheo kwa wanaume wenye matatizo ya nguvu za kiume.
 

Wanaotumia runinga kwa muda mrefu hupoteza nguvu za kiume



WANAUME wanaotumia muda wa saa tatu na zaidi kwa siku kutazama runinga wanapoteza nguvu za kiume ukilinganisha na wale wanaotazama runinga mara chache.

Utafiti uliofanywa na Chuo Kikuu cha Afya ya Umma cha Havard (HSPH) kilichopo Boston nchini Marekani, umebaini kuwa kuporomoka kwa kiwango cha mbegu za kiume kunahusiana moja kwa moja na kutofanya mazoezi na kutazama runinga kwa muda mrefu.

Imeelezwa kuwa wanaume wanaotazama runinga kwa zaidi ya saa 20 kila wiki wanapoteza asilimia 44 ya mbegu za kiume ukilinganisha na wale wasiotumia muda mrefu katika runinga.

Vilevile, wanaume wanaofanya mazoezi kwa zaidi ya saa 15 kwa wiki, wana uwezo wa kuongeza asilimia 73 ya mbegu zao ukilinganisha na wale wasiofanya mazoezi au wanaofanya mazoezi chini ya saa tano kwa wiki.

Kiongozi wa utafiti huo, Dk Audrey Gaskin alisema mtindo wa maisha unachochea zaidi upungufu wa mbegu za kiume na uzalishwaji wa mbegu za kiume.

Mtafiti huyo alifanya uchunguzi wa viwango vya mbegu za kiume za wanaume 189 wenye umri wa kati ya miaka 18 na 22 kuanzia mwaka 2009 hadi 2010.

Wanaume hao walihojiwa kuhusu kiwango cha ufanyaji wao wa mazoezi, muda wanaotumia katika kutazama runinga au filamu katika kipindi cha miezi mitatu.

“Baada ya utafiti huo, nusu ya wanaume wasiofanya mazoezi na waliotumia muda mrefu katika runinga walikuwa na kiwango hafifu cha uzalishaji wa mbegu,” alisema Dk Gaskin.
Dk Gaskin alisema: “Masuala mengine ya kiafya yanayoweza kuathiri kiwango cha mbegu za kiume ni chakula, msongo wa mawazo na uvutaji wa sigara,” alisema.

Daktari huyo alisema mwanamume anapokaa kwa muda mrefu katika sofa mbegu za kiume zinapata kiwango kikubwa cha joto ambalo huathiri uzalishwaji wa mbegu.
Alisema wanaume wanaohitaji watoto wanatakiwa kuacha kuvaa nguo za ndani zinazobana ili kuimarisha kiwango cha mbegu za kiume huku madereva na waendesha baiskeli wakionywa kuwa katika hatari ya kupungukiwa kutoa mbegu nyingi.

Mhadhiri Mkuu katika Chuo Kikuu cha Sheffield nchini Uingereza, Dk Allan Pacey anasema matokeo ya utafiti wake yatasaidia kuelimisha umma.

Hata hivyo, Daktari bingwa wa Uchunguzi wa Magonjwa kwenye Kitengo cha Patholojia katika Hospitali ya Muhimbili, Henry Mwakyoma aliyewahi kufanya utafiti kuhusu ugumba kwa wanaume, alisema bado utafiti wa Dk Gaskin una maswali mengi.

“Siwezi kuukubali au kuukataa utafiti wake, inawezekana ni mionzi au joto ndilo linalosababisha udhaifu wa mbegu hizo, lakini bado utafiti wake una maswali mengi,” alisema Dk Mwakyoma.